Social Icons

Tuesday 4 October 2016

TUME YA UCHAGUZI YAANDAA PROGRAMU YA ELIMU YA MPIGA KURA VYUO VIKUU NCHINI

Kwa wanavyuo wote watanzania popote Duniani Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255629914471. insta : @matukionawanavyuo Tumieni mtandao huu ni wenu nyote. 
Hussein Makame, NEC
Tume ya Taifa ya Uchaguzi imeandaa programu ya kutoa elimu ya mpiga kura katika vyuo vikuu nchini ili kutoa fursa kwa wanavyuo kufahamu taratibu na Sheria zinazoongoza uchaguzi.
Hayo yamesemwa na Mkurugenzi wa Uchaguzi wa tume hiyo Bw. Kailima Ramadhani, wakati akitoa tathmini ya utekelezaji wa mkakati wa kutoa elimu ya mpiga kura nchini juzi jijini Dar es Salaam jijini.
Alisema program hiyo itaanza kwa kutoa elimu hiyo kwenye Chuo Kikuu cha Dodoma, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na baadaye kutoa elimu hiyo kwenye vyuo vingine nchini.
Mkurugenzi Kailima alieleza programu hiyo kufafanua mikakati ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi kuhakikisha kuwa inatoa elimu ya mpiga kura kwa makundi mbalimbali nchini ambayo kwa sasa inatolewa kwa wanafunzi wa shule za Sekondari nchini.
 “Lakini niseme vyuo vikuu hatujavisahau kwa sababu tuna program hivi sasa kwamba tumepanga tutakapokwenda vyuo vikuu, tutakwenda Chuo Kikuu cha Dodoma na chuo kingine” alisema Bw. Kailima na kuongeza kuwa:
“Lakini tuna mpango wa kwenda Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na vyuo vingine vyote tuzungumze nao, labda niseme hapa kwamba hatwendi kuzungumza kuhusu uhalali wa katiba au sheria zilizopo”
“Tunakwenda kuzungumza katiba ya sasa inasemaje kuhusu taratibu za uchaguzi na utaratibu mzima na mfumo wake ukoje, tunakwenda kuzungumza Sheria za sasa za Uchaguzi”
Bw. Kailima aliweka wazi kuwa asingependa mikutano hiyo na vyuo vikuu kujadili kuhusu katiba bali kuzungumzia Sheria zinazoiongoza tume kusimamia na kuratibu uchaguzi.
“Wewe ukiwa na hoja yako ya katiba sio hii, hiyo ina jukwaa lingine watakuja wenye jukwaa lao kuzungumzia suala hilo lakini sisi tunakuja kukwambia Sheria inasema Tume isimamie na kuratibu uandikishaji wa wapiga kura kwa ajili ya uchaguzi wa Rais na wabunge kwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania” alisema.
Alieleza kuwa Tume iliona umuhimu wa kuanza kutoa elimu hiyo kwa ngazi ya sekondari ili kuwawezesha wanafunzi wa ngazi hiyo kupata elimu ya mpiga kura mapema na kuepusha vurugu zinazotokana na kukosekana kwa uelewa wa taratibu za uchaguzi.
 “Unajua haya mambo kama hamyazungumzi mapema ndio baadaye mnakuja kuyaona ni mageni, yanaleta vurugu watu wanakatana mapanga lakini ikiwa ni kitu cha kawaida na kinazunguzika vurugu zinakwisha” alifafanua Bw. Kailima.
Aliongeza kuwa wanafunzi wa shule za sekondari ndio wagombea wa Urais na ubunge watarajiwa na ni wenyeviti, makatibu na wajumbe wa vyama vya siasa watarajiwa na wakipata elimu mapema itawajenga kujua Sheria ya Uchaguzi.
“Yule wa chuo kikuu tayari ni mjumbe wa chama fulani, mwingine tayari ni mgombea, ueleweshaji wake utakuwa sio mgumu kuliko yule wa shule ya sekondari” alisema.
Tume ya Taifa ya Uchaguzi mbali na kutoa elimu ya mpiga kura kwa wanafunzi wa shule za Sekondari nchini, imepanga kuanzisha klabu za uchaguzi katika shule hizo ili kukuza uelewa wa masuala mbalimbali ya uchaguzi kwa wanafunzi wa ngazi hiyo.
Sanjari na kutoa elimu hiyo kwa shule za sekondari, NEC pia inashiriki katika maonesho na mikutano mbalimbali nchini ili kukutana na wananchi ana kwa ana na kuwapa elimu hiyo.
Mwisho


No comments: