Social Icons

Wednesday 15 November 2017

VIONGOZI TAASISI FEKI MIKOPO ELIMU YA JUU MBARONI

Kwa wanavyuo wote watanzania popote Duniani Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. insta : @matukionawanavyuo Tumieni mtandao huu ni wenu nyote. 

Imeandikwa na Magnus Mahenge, 
Mkurugenzi Mkuu wa taasisi ya Tanzania Social Support Foundation (TSSF) Donati Salla (kushoto) akifafanua jambo kwa waandishi wa habari (hawapo pichani) kabla ya kutiwa mbaroni jana
SERIKALI imeviagiza vyombo vya ulinzi na usalama kulichunguza Shirika la Tanzania Social Support Foundation (TSSF) kutokana na kudaiwa kuwahadaa Watanzania linatoa mikopo na wanafunzi 198 wakarubuniwa kwamba watapewa mikopo ya zaidi ya Sh milioni 533.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia na Mafunzo ya Ufundi, William Ole Nasha pia amepiga marufuku shirika hilo kujihusisha na utoaji mikopo na amezifunga akaunti zake zote baada ya kujiridhisha hakuna hata chembe ya shirika hilo kuwa na uwezo wa kutoa mikopo.
“Naviagiza vyombo vya usalama kuwakamata na kuwahoji viongozi wa shirika hili, kuwauliza ukweli kuhusu huduma za utoaji mikopo na kujiridhisha kuhusu mkakati wa kuwaibia na sheria ichukue mkondo wake,” alisema Waziri.
Alisema shirika hilo ni la kitapeli kutokana na kuwatoza wanafunzi Sh 30,000 kila mmoja za kujisajili wakati haina fedha kwenye akaunti. Alisema viongozi wa shirika hilo wamesema walitegemea kupata fedha kutoka Kampuni ya Cagney la Marekani ambapo kwanza walitakiwa kutoa dola 50,000 ili wawape ufadhili huo.
Mkurugenzi wa shirika hilo, Donati Salla alikiri kuwatoza wanafunzi Sh 30,000 na akaahidi kuzirudisha mapema Serikali itakavyoagiza na wapo tayari kuendelea kutoa usajili bure kwa wanafunzi kwa lengo la kuwasaidia Watanzania.
Ofisa Utawala, Marwa Charles alisema shirika lao si la kiserikali, hivyo si lazima liwe na fedha linapotoa huduma na si lazima lioneshe kiwango cha fedha kilicho benki bali linatoa huduma tu.
Charles alisema kulikuwa na matatizo katika shirika hivyo wakachelewa kutuma dola 50,000 za Marekani sawa na Sh milioni 112 Novemba 12, mwaka huu nchini Marekani ili wapate fedha za kukopesha wanafunzi 50,000.
Waziri Ole Nasha alisema shirika hilo ni la kitapeli kwa sababu limetumia fursa ya uhitaji wa mikopo kwa wanafunzi kudanganya ambapo wanafunzi 600 waliomba mikopo wakati likijua halina fedha zaidi ya Sh milioni 60 au 70 tu.
“Shirika hilo ni la kitapeli”, Ole Nasha alisema na kuongeza katika mkataba na Kampuni ya The Cagney ya Marekani, hakuna mahali popote palipoonesha itatoa fedha kuwafadhili wanafunzi, badala yake viongozi walikuwa wakiulizia uwezekano wa kufanya harambee.
Waziri ole Nasha alisema katika mkutano na viongozi wa taasisi hiyo, alisema wamebaini TSSF haina uwezo wa kutoa mikopo kwa wanafunzi 50,000, bali ulikuwa utapeli wa kupata Sh 30,000 za ada za kujiandikisha.
Alisema hakuna sehemu ya kupata fedha na serikali inatoa taarifa kwa umma ufahamu shirika hilo halina uwezo wa kutoa mikopo kwa wanafunzi waliokwishaanza masomo vyuoni wakitegemea kupata mikopo Desemba 20, 2017.
Japo taasisi hiyo ilisajiliwa kihalali nchini, serikali imebaini kwamba bajeti yake kwa mwaka ni Sh milioni 2.5, hivyo kusingekuwa na miujiza kuwa na uwezo wa kuwa na fedha za kutosha kufadhili wanafunzi 50,000 kwani historia haioneshi uwezo huo wa kifedha.
Alisema shirika hilo lilikuwa na nia mbaya ya kuwahadaa wanafunzi na lilidai wangekosa fedha Marekani, wangepata China ambako pia hakuna mkataba wa makubaliano ya fedha.
Wanafunzi 198 walioahidiwa mikopo na shirika hilo walikuwa wameomba kusoma vyuo vikuu vya Dar es Salaam (UDSM), Nyegezi (SAUT), Chuo Kikuu cha Tiba Muhimbili (MUHAS), Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine (SUA), Morogoro na vingine walitozwa Sh 30,000 za kusajiliwa jumla yake ikiwa Sh milioni 5.94.
Kutokana na uhaba wa mikopo ya wanafunzi katika Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu (HESLB), zaidi ya wanafunzi 600 walikuwa wameahidiwa watapewa mikopo na shirika hilo na kurudisha fedha kwa riba ya asilimia sita.
Naibu Waziri ole Nasha alisema, serikali itaangalia namna ya kuwasaidia wanafunzi hao waliotapeliwa na shirika hilo kwani wanaweza kushindwa kuendelea na masomo yao kwa sasa.
Mkutano na waandishi wa habari ulipomalizika, viongozi wa shirika hilo, Salla na Charles walikamatwa na kuwekwa chini ya ulinzi wa Polisi kwenda kutoa maelezo kuhusu nia hiyo ya kutapeli wanafunzi wenye shida ya mikopo.
CHANZO HABARI LEO

No comments: