TUME ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU) imetangaza kufungua maombi kwa
awamu ya pili ya udahili wa wanafunzi wanaotarajiwa kujiunga na masomo
ya shahada za awali kwa mwaka wa masomo wa 2017/18, baada ya kubainika
waombaji wengi hawakuchaguliwa kutokana na sababu mbalimbali.
Awamu ya kwanza ya udahili huo ilimalizika tangu Agosti 30, mwaka huu
na uhakiki wa majina ya waombaji wanaotaka kujiunga na vyuo vya elimu
ya juu kukamilika. Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Kaimu Katibu
Mtendaji wa tume hiyo, Profesa Eleuther Mwageni jana, awamu hiyo ya pili
ya maombi ya udahili inaanzia rasmi tangu jana na itakamilika Oktoba
10, mwaka huu.
Profesa Mwageni alisema tume hiyo imechukua hatua hiyo ya awamu ya
pili ya udahili ili kuruhusu udahili kwa waombaji waliokosa nafasi
kwenye awamu ya kwanza, waombaji wa kidato cha sita walioshindwa kuomba
awamu ya kwanza na waombaji wenye vigezo vya Stashahada walioshindwa
kupata namba ya uhakiki wa tuzo (AVN).
Aidha, alitaja sababu nyingine za awamu hiyo ya pili ya udahili kuwa
ni kuruhusu udahili kwa waombaji waliomaliza mitihani ya Cambridge mwaka
huu na matokeo yao yameshatoka na wanafunzi wa vyuo vikuu watakaokuwa
na uthibitisho kutoka vyuo vya awali.
Kwa mujibu wa ratiba ya TCU, kwa sasa iko katika hatua kutangaza
udahili wa wanafunzi watakaojiunga na vyuo vya elimu ya juu, hatua
iliyokamilika Oktoba 2, mwaka huu. Baada ya hapo, ratiba hiyo imeonesha
kuwa imetoa muda kwa ajili ya wanafunzi wanaoomba uhamisho, utaratibu
utakaochukua muda wa siku 20 na kukamilika rasmi Novemba 30 kupisha
uhakiki wa wanafunzi waliodahiliwa kwenye vyuo vyote vya elimu ya juu
nchini utakaofanyika Desemba Mosi, mwaka huu.
Hata hivyo, hivi karibuni mwaka huu TCU ilitangaza kubadili mfumo wa
udahili ambapo kuanzia mwaka 2017/18 maombi ya kujiunga na elimu ya juu
yanatumwa moja kwa moja vyuoni. TCU imepanga Oktoba 30, mwaka huu kuwa
siku ya kufunguliwa kwa vyuo vyote vinavyotoa elimu ya juu.
Kwa mujibu wa Profesa Mwageni, Tume hiyo haitopokea maombi ya
kujiunga na vyuo vikuu kama ilivyokuwa hapo mwanzo na kwamba utaratibu
wa kutuma maombi ni ule ule uliotumika katika awamu ya kwanza ya
udahili.
April 15, mwaka huu, wakati akizindua hosteli za wanafunzi wa Chuo
Kikuu cha Dar es Salaam, Rais John Magufuli aliiagiza TCU kutowachagulia
vyuo wanafunzi wa elimu ya juu na kuwaacha wajichagulie wenyewe vyuo
wanavyovitaka.
CHANZO HABARI LEO
No comments:
Post a Comment