Social Icons

Tuesday 29 August 2017

CHUO KIKUU DAR NI DARAJA AEC

Kwa wanavyuo wote watanzania popote Duniani Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. insta : @matukionawanavyuo Tumieni mtandao huu ni wenu nyote. 

 Imeandikwa na Lucy Ngowi
Ukumbi wa Nkurumah ndio kielelezo cha Chuo Kikuu cha Dar es Salaam
UONGOZI wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, moja ya vyuo vikongwe na vyenye heshima kubwa katika Ukanda wa Afrika Mashariki, umesema una mikakati mingi ya kukifanya kuendelea kuwa bora ndani ya Ukanda husika, Afrika na duniani kwa ujumla, ili kiendelee kuwa daraja la kielimu.
Aidha, kimesema kama kilivyotoa wasomi bora wanaoendelea kushika nyadhifa mbalimbali ndani na nje ya Afrika, bado kinaendelea na kitaendelea kutoa wasomi walioiva kwa soko la ajira.
Hayo yamesemwa na Mkurugenzi wa Huduma kwa Umma wa chuo hicho, Dk Mona Mwakalinga. “Chuo Kikuu Dar es Salaam kinazalisha viongozi wanapotoka hapa, ndiyo maana kimetoa marais wa nchi mbalimbali, mawaziri wakuu, wakuu wa taasisi za kimataifa, na wengine wengi, hakika orodha ni ndefu.
“Hiki ni chuo pendwa Tanzania na Afrika Mashariki, ni sehemu ambayo ni chaguo la kwanza la wanafunzi kabla ya kuomba vyuo vingine,” alisema Dk Mwakalinga aliyeongeza kuwa, chuo kina Kurugenzi ya Ushirikiano wa Kimataifa ambayo inahakikisha inakiuza chuo ndani na nje ya nchi ili kipate walimu na wanafunzi.
Amesema mwanafunzi anapomaliza masomo yake chuoni hapo anaweza kuuzika katika nchi za Afrika Mashariki na ulimwenguni pote. Dk Mwakalinga alisema hayo alipokuwa akizungumza na Habari Leo kuhusu uhusiano wa chuo hicho na wanafunzi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki wanaomaliza chuoni hapo.
Alisema mwanafunzi yeyote anayetoka UDSM, anaweza kwenda vyuo vikuu vya Nairobi nchini Kenya ama Kampala nchini Uganda na kuendelea na masomo yake. “Katika Afrika Mashariki tuna umoja wa kushirikishana wanafunzi na walimu.
UDSM tunatoa taaluma ambayo mtu akitoka chuoni hapa anaweza kwenda Nairobi kuendelea na masomo,” alisema na kuongeza kuwa pia kinamsaidia mwanafunzi anayesoma hapo kuuzika Afrika Mashariki na kwingineko.
Alisisitiza kuwa chuoni hapo milango ipo wazi kwa wanafunzi wote, pia kuna walimu wanatoka hapo na kwenda kufundisha vyuo vingine vya Afrika Mashariki na walimu wa nchi za Afrika Mashariki wanakuja chuoni hapo kufundisha.
Alisema chuo kimekuwa kinapokea wanafunzi kutoka Kenya, Uganda, Burundi na nchi nyingine zenye makubaliano maalumu, ikiwemo Angola. Chuo hicho, kimetoa marais, wakiwemo Jakaya Kikwete aliyeiongoza Serikali ya Awamu ya Nne Tanzania, na Dk John Magufuli, rais wa sasa.
Wengine ni Yoweri Museveni wa Uganda, Rais wa zamani wa Benki ya Maendeleo Afrika (AfDB), DK Donald Kaberuka ambaye ni raia wa Rwanda, Mwanasheria Mkuu wa zamani wa Kenya, Willy Mutunga, John Garang, Makamu wa Kwanza wa Rais wa Sudan.
Pia kimetoa Mawaziri wakuu wanne wa Tanzania, Kassim Majaliwa aliyepo madarakani, Joseph Warioba, Mizengo Pinda na Edward Lowassa. Aliyekuwa Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Dk Asha Rose-Migiro pia ni miongoni mwa matunda ya UDSM, kama ilivyo kwa Eriya Kategaya, Naibu Waziri Mkuu wa Uganda aliyekuwa pia Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki. Orodha ni ndefu, lakini UDSM kinaahidi kuendelea kuibua wasomi na watendaji katika taasisi mbalimbali zenye kiwango cha kimataifa.
CHANZO HABARI LEO

No comments: