Social Icons

Friday 17 June 2016

MUHAS kutoa huduma za kliniki kwa wenye selimundu

Kwa wanavyuo wote watanzania popote Duniani Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. Tumieni mtandao huu ni wenu nyote. 

CHUO Kikuu cha Sayansi na Tiba Muhimbili (MUHAS), kimesema kitaanza kutoa huduma za kliniki kwa wagonjwa wa selimundu katika hospitali za mikoa nchini. Awali, huduma hizo zilizokuwa zikitolewa na Hospitali ya Rufaa ya Muhimbili zilisitishwa baada ya kuzidiwa wagonjwa.
Mratibu wa magonjwa hayo kutoka MUHAS, Dk Deogratius Soka, alisema kwa kuanzia tayari katika Hospitali ya Temeke kliniki imekamilika na kuanza kutoa huduma na wanaendelea kuandaa katika hospitali za mikoa za Amana na Mwananyamala jijini Dar es Salaam kisha kwenda mikoa mingine.
“Huduma za kliniki katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH), hazikusitishwa bali zilipotoshwa kwani wingi wa wagonjwa ulifanya tutawanye huduma mikoani kwa kuanza kufanya kliniki na Muhimbili kubakisha wagonjwa wanaohitaji msaada zaidi,” alisema.
Alisema, kwa kawaida watu wenye ugonjwa huo wanatakiwa kuonana na madaktari katika kliniki zao maalumu kila baada ya miezi mitatu, lakini katika Hospitali ya Muhimbili walikuwa wakifika kila baada ya zaidi ya mwaka kutokana na wingi wa wagonjwa.
Dk Soka alisema, katika ujenzi wa maandalizi ya kliniki hizo wataangalia maeneo yenye wagonjwa wengi zaidi na kisha kuendelea mikoa mingine kutokana na kuwa serikali wameuingiza ugonjwa huo katika magonjwa yasiyoambukizwa hivyo kusamehewa katika matibabu au kuchagia kidogo.
Alisema, mikoa ya ukanda wa Pwani kama Mtwara, Lindi, Pwani na Dar es Salaam pamoja na ile ya Kanda ya Ziwa kama Mwanza ,Shinyanga na mingineyo ndiyo inaongoza kwa kuwa na idadi kubwa ya watu wenye ugonjwa huo.
Alisema Tanzania ni nchi ya tano duniani kwa watu wake kuwa na ugonjwa huo wakifuatiwa na India, Nigeria, Congo na Algeria, hivyo ugonjwa huo kuwa na athari kubwa katika jamii kutokana na uelewa mdogo.
Alisema, baadhi ya watu wana imani potofu kuwa watoto wenye ugonjwa huo hawawezi kuishi zaidi ya miaka 18, jambo analoeleza kuwa si kweli. Pia, alisema upotoshaji mwingine ni kwamba mtoto mwenye ugonjwa huo akifikisha umri wa miaka hiyo 18 hupona. Anafafanua kuwa anayepata ugonjwa huo huishi nao kwa miaka yote na ana uwezo wa kuwa hai mpaka kufikia uzee.

No comments: