Social Icons

Tuesday 11 March 2014

INASIKITISHA: MWANAFUNZI WA CHUO CHA UHASIBU CHA SINGIDA DORRYCE AFARIKI KWA KUPIGWA NA RISASI

Stori: Makongoro Oging’ na Harun Sanchawa
MAJONZI, huzuni na masikitiko vimeikumba familia ya Lwena kufuatia mtoto wao mpendwa Dorryce Lwena (27) kufariki dunia kwa kupigwa risasi mkono wa kushoto na ubavu wa kushoto na watu wasiojulikana, Uwazi lilifuatilia.

Jeneza lenye mwili wa Dorryce Lwena.
Tukio hilo la kusikitisha lilitokea mwanzoni mwa mwezi huu, saa tatu usiku, Uwanja wa Edosi, Kitunda, Ilala hatua chache kutoka nyumbani kwa marehemu huyo.
Siku ya tukio, Dorryce ambaye ni mwanafunzi wa Chuo cha Uhasibu Singida (DSA), alikuwa akitoka Kariakoo kununua vifaa vya kwenda navyo chuo siku mbili mbele lakini kifo kilimkuta akiwa anakaribia kufika nyumbani.
Mama mzazi wa Dorryce akiwa na simanzi wakati wa mazishi ya mwanaye.
Kama ilivyo ada, baada ya kujulishwa tukio hilo la kikatili, waandishi wa Uwazi walifika eneo la tukio na kufanya mahojiano na baba wa kufikia wa marehemu ambaye alikuwa akiishi naye baada ya baba mzazi kutengana na mama yake.
Baba huyo aliyejitambulisha kwa jina moja la Maganga alikuwa na haya ya kusema:
“Ilikuwa Jumamosi, Machi Mosi, mwaka huu, saa tatu usiku nikiwa karibu na kwangu, mke wangu (mama wa marehemu) alinipigia simu akaniambia kuna risasi zimepigwa karibu na nyumba yetu, nikamwambia haraka sana wafunge milango na mtu asitoke nje hadi itakapojulikana kuwa risasi hizo zilikuwa za nini.

Ndugu na jamaa wa marehemu wakilia kwa uchungu wakati wa mazishi.
“Muda mfupi baada ya kuongea na mke wangu, dada wa Dorryce alinipigia simu akiniambia nirudi nyumbani haraka kwani Dorryce amepigwa risasi na amefariki dunia.
“Nina gari, niliingia ndani yake haraka tayari kwa safari ya kurejea nyumbani. Nikiwa nakaribia nyumbani niliona kundi la watu, nilisogelea eneo hilo na kukuta mwili wa Dorryce umelala katika dimbwi la damu.
“Nilikuta familia yangu, akiwemo mama wa marehemu wakilia kwa uchungu. Iinibidi nikatoe taarifa Kituo Kidogo cha Polisi Kitunda, nao walinishauri niende Kituo cha Polisi Stakishari.


“Polisi walifika eneo la tukio na kufanya michoro kisha wakauchukua mwili hadi Hospitali ya Taifa Muhimbili.
“Mke wangu ana hali mbaya sana jamani. Tangu tukio hilo amekuwa akizimia mara kwa mara, presha inapanda na kushuka. Naombeni msimhoji,” alisema kwa masikitiko makubwa baba huyo.
Alisema mpaka siku hiyo familia ilikuwa haijui chanzo cha mauaji hayo.

Akasema: “Ninachokumbuka mimi siku hiyo mke wangu alimkataza marehemu asiende Kariakoo lakini alikataa, akasema kwa vile Jumapili atakwenda kanisani na Jumatatu ndiyo safari ya kurudi chuo, afadhali aende siku hiyo.”
“Ila wakati marehemu yupo chuoni alizaa na mwanaume mmoja ambaye tulimtaka amhudumie mtoto kwa vile mama yake bado anasoma lakini alikataa, hivyo marehemu aliamua kumchukua mtoto na kumpa. Hadi hapo tukawa hatuna uhusiano naye mzuri,” alisema mzee huyo.
Waandishi wetu walifanya mahojiano na majirani kutaka kusikia kama wanajua lolote juu ya tukio hilo ambapo baadhi yao walisema mauaji hayo hayajawahi kutokea eneo hilo na kudai kwamba marehemu  ndiye anayejua sababu ya kupigwa risasi.
Marehemu wakiti akiwa hai

“Marehemu baada ya kupigwa risasi ya kwanza alilia kwa uchungu na kupiga kelele kuomba msaada. Hata hivyo, hakuna aliyejitokeza.
“Aliongezwa risasi ya pili sauti yake haikutokea tena, wale watu walitimka na pikipiki ndipo wananchi tukajitokeza, nahisi ni mapenzi,” alisema mwanamke mmoja anayefanya biashara karibu na eneo la tukio.
Baba mzazi aliyejitambulisha kwa jina la Julius Jacob Lwena anayeishi Tabata Tenge, Dar yeye alikuwa na haya ya kusema:

“Kifo cha Dorryce kimeniuma sana, ila napenda kusema kwamba maisha yake kwa undani siyajui sana kwa sababu nilikuwa mbali naye.
“Mara ya kwanza marehemu alipomaliza elimu ya sekondari alijiunga na Chuo cha Polisi Moshi, alirudishwa kutokana na ujauzito.

“Baada ya kujifungua tulimpeleka Chuo cha Utumishi Singida, bahati mbaya akapata mimba ya mwanaume mwingine, ikabidi arudi nyumbani.
“Baada ya kujifungua tulimpeleka chuo cha uhasibu Singida na mauti yamempata alipokuja likizo,” alisema mzee huyo.

Marehemu alizikwa Machi 4, mwaka huu katika Makaburi ya Tabata Segerea jijini Dar. Mungu ailaze pema peponi roho yake. Amina.

CHANZO: GLOBAL PUBLISHERS

No comments: