Mtunzi
wa kitabu cha ‘Safari Ya Ndoto’ Bw. Aman Nguku (kulia) ambaye pia ni
mwanafunzi wa chuo cha Ardhi akiwaelezea waandishi wa habari na wageni
waalikwa (hawapo pichani) kuhusu kitabu hicho alichokizindua jana jijini
Dar es Salaam. (Picha na Atuza Nkurlu)
Bi.
Kikwa (kushoto) na Bw. Mallewo wakionyesha kitabu cha ’Safari Ya
Ndoto’ alichokiandika mtoto wao Aman (katikati) anayesoma shahada ya
uchumi mwaka wa tatu katika chuo kikuu cha Ardhi.
Mtunzi
wa kitabu cha ‘Safari Ya Ndoto’ Aman Nguku akihojiwa na waandishi wa
habari katika uzinduzi wa kitabu hicho jana. Wanaoshuhudia ni walezi
wake Bi. Kikwa na Bw. Mallewo.
Vijana
wakitanzania wameaswa kuacha kulalamika na kuishi katika maisha ya
nadharia, badala yake wameshauriwa kubadilika kuwa watendaji na wenye
uthubutu wa kutimiza malengo yao katika maisha.
Maneno hayo
yalisemwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Amajat Investment Bw. Aman
Nguku jijini Dar es Salaam jana katika uzinduzi wa kitabu chake
kiitwacho ‘Safari Ya Ndoto’ inayobeba kauli mbiu “Sio Serikali ni Mimi, Wewe na Sisi.”
Akizungumza
na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, Bw. Nguku alisema imefika
wakati sasa watanzania hasahasa kundi la vijana waamke kutoka usingizini
na kutimiza malengo yao ya kimaisha ambayo wanapenda kufikia.
“Imetosha
kusema kesho, kufikiri bila kutenda na kuongea bila vitendo.
Kinachotakiwa ni kuanza utekelezaji,” alinukuu Bw. Nguku kutoka kwenye
kitabu chake chenye kurasa 108.
Akielezea
madhumuni ya kuandika kitabu hicho, Bw. Nguku ambaye pia ni mwanafunzi
wa mwaka wa tatu anayesomea shahada ya Uchumi katika Chuo Kikuu cha
Ardhi jijini Dar es Salaam alisema:
“Hiki
kitabu ni mahususi kwa wale watu ambao wana ndoto mbali mbali katika
maisha yao lakini hawajui pakuanzia, iwe ndoto ya kuwa mfanyabiashara
maarufu, mwanasiasa au daktari bingwa. Hiki kitabu ni ramani maalum
kwao.”
Aliendelea,
“Kitabu hiki kinaweza pia kuwa changamoto kwa wale ambao wamekata tamaa
katika maisha. Kwa kusoma maandishi ya kitabu hiki, wanaweza wakafufua
ndoto zao na kufanikiwa katika yale waliyoyapanga.”
‘Safari Ya Ndoto’ pia
inabeba dondoo kutoka kwa Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere,
mfanyabiashara maarufu Bw. Reginald Mengi na Mkurugenzi Mtendaji wa
Helvetic Solar Contractors Bw. Patrick Ngowi.
Kitabu hiki
kinasambazwa katika maduka mbali mbali jijini Dar es Salaam na nchi
nzima ili watanzania wengi wapate kukisoma. Kinauzwa kwa Tsh 5000 tu.
Kwa sasa, mtunzi Nguku pia anaandika vitabu vingine viwili venye vichwa ‘Ndogo lakini muhimu, kesho’ na ‘What is life for!’(Maisha ni ya nini!).
1 comment:
BIG UP braza
Post a Comment