Social Icons

Thursday 10 November 2016

SERIKALI KUKIBORESHA CHUO CHA OLMOTONYI

Kwa wanavyuo wote watanzania popote Duniani Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. insta : @matukionawanavyuo Tumieni mtandao huu ni wenu nyote.


Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe. Prof Jumanne Maghembe akijibu hoja mbalimbali za wabunge katika kikao cha tisa cha mkutano wa tano wa Bunge la 11linaloendelea Mjini Dodoma Novemba 10, 2016.


Na Jacquiline Mrisho – MAELEZO, Dodoma.

Serikali imejipanga kuboresha miundo mbinu ya Chuo cha Misitu cha Olmotonyi kilichopo katika Jimbo la Chambani Mkoa wa Kusini Pemba ili kuwavutia wanafunzi kujiunga na chuo hicho hivyo kuongeza idadi ya wataalamu wa misitu nchini.

Hayo yamesemwa leo mjini Dodoma na Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Prof. Jumanne Maghembe alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Chambani Mhe. Yussuf Hussein lililohoji juu ya mpango wa Serikali kukiboresha chuo hicho.

Prof. Maghembe amesema kuwa wameamua kuboresha miundo mbinu ya chuo hicho kwa sababu kumekuwa na upungufu mkubwa wa wataalamu wa misitu nchini ambapo kwa sasa kila mtaalamu wa misitu anasimamia jumla ya hekta 25,000 za misitu kinyume na uwiano unaokubalika kimataifa wa mtaalamu mmoja kusimamia hekta 5000.

”Serikali yetu kwa kushirikiana na Serikali ya Norway inaendelea kutekeleza mradi wa Kuwezesha Jamii kupitia Mafunzo ya Shughuli za Usimamizi Shirikishi wa Misitu pamoja na Mabadiliko ya Tabianchi, mradi ambao tuna uhakika utakijengea chuo uwezo na kukiboresha zaidi”, alisema Mhe. Maghembe.


Mhe. Maghembe ameyataja malengo ya mradi huo kuwa ni kukarabati nyumba saba za watumishi, kuimarisha maktaba ya chuo kwa kuweka samani, vitabu 137 vya mada 22 tofauti, kuweka vifaa 62 vya kufundishia, kompyuta 15 na kutoa mafunzo ya kompyuta kwa wakutubi watano, ukarabati wa mtandao wa mawasiliano pamoja na kuunganisha Chuo na mkongo wa Mawasiliano wa Taifa.

Mhe. Prof Maghembe ameongeza kuwa mradi huo unaendelea na ujenzi wa bweni moja lenye uwezo wa kuchukua wanachuo 100 na ukumbi wa mihadhara wenye uwezo wa kuchukua wanachuo 200 kwa wakati mmoja.

Aidha, mradi huu utawajengea uwezo wa mbinu bora za kufundishia wakufunzi 16 na kutoa mafunzo kwa jamii za vijijini kuhusu kuhifadhi misitu na shughuli mbadala za kiuchumi.

Mhe. Maghembe amefafanua kuwa katika kipindi cha miaka mitatu  kutoka mwaka 2013 hadi  2016 Wizara kupitia Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania imegharamia ukarabati wa nyumba 9 za watumishi, kumbi za chakula kugharamia mikutano na ununuzi wa kompyuta mbili na gari aina ya Tata kwa ajili ya usafiri kwa mafunzo ya vitendo nje ya Chuo pia kupitia mradi huo Serikali inatoa ufadhili kwa wanafunzi wa ngazi ya Astashahada na Stashahada.



No comments: