Social Icons

Friday 20 May 2016

Wadaiwa 21,721 wajitokeza HESLB kurejesha mikopo

Kwa wanavyuo wote watanzania popote Duniani Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. Tumieni mtandao huu ni wenu nyote.
Na FATMA SALUM -MAELEZO
Jumla ya wadaiwa wapya 21,721 wa mikopo ya elimu ya juu wamejitokeza ili kuanza kulipa madeni yao kufuatia agizo la siku 60 lililotolewa na Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) mnamo Machi 14 mwaka huu.

Hayo yamesemwa na Mkurugenzi wa Urejeshaji Mikopo kutoka Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) Bw. Robert Kibona wakati akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam kuhusu tathmini ya agizo lililotolewa  na bodi hiyo kwa wanufaika wa mikopo na waajiri ili kutimiza wajibu wao kisheria.

Bw. Kibona alifafanua kuwa jumla ya Shilingi bilioni 151.5 zinatarajiwa kurejeshwa na wadaiwa hao ambao walikopeshwa ili kuwawezesha kupata elimu yao ya juu katika vyuo mbalimbali ndani na nje ya nchi kuanzia mwaka 1994.

Lengo la agizo lilikuwa ni kuhahakisha madeni yote yaliyoiva yanakusanywa ili kuongeza uwezo wa kukopesha watanzania wengi zaidi na agizo hili limeisha Mei 13 mwaka huu.” alisema Bw. Kibona

Kwa mujibu wa Bw. Kibona, kati ya wadaiwa waliopatikana, wadaiwa 19,528 walipatikana baada ya Bodi kuchambua taarifa za waajiriwa zilizowasilishwa na waajiiri na wadaiwa wengine wapatao 2,007 walijitokeza kwa hiari.

“Waajiri wana wajibu wa kisheria wa kuwasilisha taarifa za waajiriwa wao, baadhi yao walifanya hivyo katika siku hizo sitini na tukawabaini wadaiwa hao, tunawapongeza waajiri kwa ushirikiano walioutoa na wanufaika wote waliojitokeza kwa hiari” alisema Bw. Kibona.

 Aidha Bw. Kibona aliongeza kuwa Bodi imeongeza siku 30 za ziada kuanzia Mei 20, 2016 kwa wadaiwa waliobaki kujitokeza na uamuzi huo umetokana na tathmini iliyoonyesha kuwa kuna idadi kubwa ya waajiri na wanufaika wanaoendelea kujitokeza.
Kwa upande wake Mkurugenzi Msaidizi Habari, Elimu na Mawasiliano wa Bodi ya Mikopo Bw. Cosmas Mwaisobwa alisema kuwa kiwango cha ukusanyaji wa madeni kwa mwezi kinatarajiwa kuongezeka kutoka shilingi bilioni 2.7 zinazokusanywa hivi sasa na kufikia shilingi bilioni 8 ifikapo mwezi Juni 2016.
Katika kipindi cha mwaka 1994/1995 hadi sasa, kiasi cha shilingi trilioni 2.44 kimetolewa kwa wanufaika 378,504 wakiwemo wanafunzi wanaoendelea na masomo yao hivi sasa ambao kwa sasa hawana wajibu wa kulipa hadi pale watakapomaliza au kusitisha masomo yao.

No comments: